Kwa mujibu wa Hadith, Ramadhani ni mojawapo ya majina ya Mwenyezi Mungu.
Kitabu cha “Kanz al-Maram fi Amal Shahr al-Siyam” kinaashiria majina na vifungu 20 ambavyo Maasumin (AS) wametumia kurejea mwezi mtukufu.
1- Ramadhani
Ramadhani kwa Kiarabu inatokana na ar- Ramdha , ambayo ina maana ya joto kali. Katika Ramadhani, nuru ya rehema ya Mwenyezi Mungu huangazia mioyo ya waumini kama vile jua linavyoangazia ardhi. Pia, mioyo ya waumini inachangamshwa na kumkumbuka Mwenyezi Mungu.
Maana nyingine ya ar- Ramdha imetajwa kuwa ni kunyesha katika msimu wa vuli kwenye nchi kavu. Katika Ramadhani, mvua ya rehema ya Mwenyezi Mungu hutuliza nyoyo za waumini na kuwatakasa.
2- Jina lingine la Ramadhani ni Midhmar, ambalo lina maana ya kumfunza farasi wa mbio kwa siku 40 ili kumtayarisha kwa mbio hizo. Kipindi hiki kinaitwa Midhmar.
Mwezi wa Ramadhani waumini hufunga kwa muda wa mwezi mmoja kujiandaa na mbio za kumtumikia Mwenyezi Mungu. Imam Hussein (AS) amesema Mwenyezi Mungu amewajaalia watu na mwezi mtukufu wa Ramadhani ili watumie fursa hii kuchuana katika kuelekea peponi.
3- Jina jingine la Ramadhani ni Shahrullah (mwezi wa Mwenyezi Mungu). Mtukufu Mtume Muhammad (SAW) amesema katika Khutba yake ya Al-Shaabaniyah: “Enyi watu! Mwezi wa Mwenyezi Mungu umekujieni ukileta baraka, rehema na msamaha wa Mwenyezi Mungu.”
Hapa kuna majina mengine matano yaliyotajwa kwa ajili ya Ramadhani na Imam Sajjad (AS):
4- Shahr al-Siyam: mwezi wa kufunga
5- Shahr al-Islam: mwezi wa Uislamu
6- Shahr al-Tahur: mwezi wa usafi au utakaso
7- Shahr al-Tamhis: mwezi wa kujisafisha na kutakasika
8- Shahr al-Qiyam: mwezi wa kuamka na kumuomba Mwenyezi Mungu usiku
Mtukufu Mtume Muhammad (SAW) alitumia majina sita yafuatayo kuutaja Mwezi wa Ramadhani:
9- Shahr al-Barakah: mwezi wa baraka
10- Shahr al-Inabah: mwezi wa kurudi kwa Mwenyezi Mungu
11- Shahr at-Tawbah: mwezi wa toba
12- Shahr al-Maghfirah: mwezi wa msamaha
13 na 14- Shahr al-Atq min an-Naar na Fawz bi al-Jannah: mwezi wa kujikomboa kutoka kwa moto wa jahannam na mwezi wa kufika peponi.
Majina mawili yafuatayo yanaonekana katika dua ya usiku wa nne wa Ramadhani iliyosimuliwa kutoka kwa Mtukufu Mtume Muhammad (SAW):
15- Shahr ath-Thawab: mwezi wa malipo
16- Shahr ar-Raja: mwezi wa matumaini
Majina mawili yafuatayo yametajwa katika Khutba ya Al-Shaabaniyah:
17- Shahr as-Sabr: mwezi wa subira na nguvu
18- Shahr al-Muwasat: mwezi wa kusaidia na kuhurumiana na ndugu katika imani
Na Mtukufu Mtume Muhammad (SAW) pia aliitaja Ramadhani kwa majina haya mawili:
19-Shahr ar-Rahmah: mwezi wa rehema
20- Sayyid ash-Shuhur: mkuu wa miezi