Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu leo (Jumanne) katika kikao cha maimamu wanaoswalisha Ijumaa kote Iran amesisitiza kwamba, leo mkono wa Mwenyezi Mungu unaonekana kufuatia kuchukua muelekeo wa kimataifa kadhia ya Gaza. Ameongeza kuwa: Leo hii dunia inawatazama watu wa Gaza, wanamapambano na makundi ya muqawama kwa macho ya mashujaa.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekutaja kupata umashuhuri watu wanaodhulumiwa wa Gaza na wakati huo huo ushindi mbele ya walimwengu kuwa ni kazi na baraka za subira na imani yao na kuongeza kuwa: Katika upande mwingine, leo hii, hakuna mtu duniani anayeamini kuhusu kupata ushindi utawala ghasibu na khabithi wa Kizayuni katika vita. Kwa maoni ya watu wa dunia na wanasiasa, utawala huu ni dhalimu, usio na huruma mbwa-mwitu mfyonza damu, aliyeshindwa na kusambaratika.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha amepongeza na kupendezwa na kazi kubwa ya taifa la Yemen na serikali ya Harakati ya Ansarullah katika kuwaunga mkono wananchi wa Gaza na kubainisha kwamba, Wayemen walizigonga njia muhimu za utawala wa Kizayuni na hawakuwa na hofu kufuatia tishio la Marekani kwa sababu mcha Mungu haogopi chochote isipokuwa Mwenyezi Mungu, na hatua walioyochukua kiuhakika ni mfano wa wazi wa Jihad kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.
Ayatullah Khamenei aliendelea kueleza matumaini yake kuwa: "Kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, mapambano, muqawama na harakati hizi zitaendelea hadi ushindi."
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha akiashiria uchaguzi ujao wa Iran ametaja "mahudhurio, hamu na hatua ya watu" kuwa ni kanuni ya msingi katika Uislamu. Aidha amepongeza uaminifu, subira, busara na kujitolea kwa wananchi wa Iran.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu halikadhalika amesema kushiriki katika uchaguzi ujao nchini ni wajibu na haki ya wananchi na kuongeza kuwa, ushiriki wa wananchi katika uchaguzi huo ni jambo la lazima kwa maana halisi ya neno hilo. Bila shaka, ameendelea kusema, uchaguzi si wajibu tu, bali ni haki ya wananchi kuwa na uwezo wa kuchagua wabunge, watekelezaji wa sheria au wajumbe wa Baraza la Wanazuoni Wataalamu.
Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa, watu wa Gaza kwa kusimama kidete wameeneza Uislamu na Qur'ani Tukufu mbele ya watu wanaotafuta ukweli duniani. Amemuomba Mwenyezi Mungu aongeze fahari ya wapiganaji walio mstari wa mbele wa mapambano hususan watu na wapiganaji wa Gaza.
4194172