Akizungumza katika mkutano ulioandaliwa na Vijana Kwa Ajili ya Quds, Marzouq Ali Mohammed Al Ghanim amesema sheria zinazohusu Palestina na kutetea taifa hilo hazijabadilika nchini Kuwait.
Aidha amesema Kuwait inapinga ‘mapatano ya karne’ ambayo lengo lake ni kuzisukuma nchi za Kiarabu kuanzisha uhusiano na utawala bandia wa Israel. Ameongeza kuwa Kuwait inaamini mapatano hayo si kwa maslahi ya Wapalestina na Waarabu kwa ujumla.
“Serikali na watu wa Kuwait watabakia kuwa waungaji mkono wa Palestina katika uga wa kimataifa na wanaamini kuwa kadhia ya Palestina ni moja ya masuala muhimu ya ulimwengu wa Kiarabu,” amesema Spika wa Bunge la Kuwait.
Al Ghanim amewapongeza Wapalestina kwa kusimama kidete katika mapambano dhidi ya utawala wa Kizayuni wa Israel hasa hujuma za utawala huo dhidi ya Msikiti wa Al Aqsa na kusema hakuna shaka kuwa hatimaye watapata ushindi.
Kundi la Vijana Kwa Ajili ya Quds limeandaa mkutano huo ikiwa ni katika mkakati wake wa kuhakikisha kuwa kadhia ya Palestina inabakia hai.