Katika mazungumzo hayo, Putin amempongeza Assad kwa kushinda uchaguzi wa rais wa Syria na akaongezea kwa kusema, "matokeo ya (uchaguzi huu) yanaonyesha kuwa wananchi wana imani na wewe; na licha ya matatizo yote yaliyojiri miaka iliyopita pamoja na majanga ya miaka iliyopita, wao (wananchi wa Syria) wangali wanauhusisha na wewe mchakato wa kuboreka na kuweza kurejea katika maisha ya kawaida."
Kwa mujibu wa baadhi ya duru za baadhi, Rais Bashar al Assad wa Syria na mwenzake Vladimir Putin wa Russia walikutana na kufanya mazungumzo hayo mjini Moscow hapo jana.
Rais wa Russia amezungumzia pia kuendelea kuwepo makundi ya kigaidi nchini Syria na hatari ya ugaidi katika nchi hiyo.
Putin amesema: "juhudi zetu za pamoja zimewezesha kukombolewa eneo kuu na sehemu kubwa ya ardhi ya Jamhuri ya Syria; na hivi sasa serikali ya Syria ikiongozwa na wewe inadhibiti asilimia 90 ya ardhi ya nchi hiyo."
Kwa mujibu wa shirika la habari la Sputnik, katika mazungumzo yao hayo, marais wa Syria na Russia wamejadili pia uwepo haramu na wa kinyume cha sheria wa vikosi vya ulinzi vya nchi ajinabi katika ardhi ya Syria.
Kwa upande wake, Rais Bashar al Assad wa Syria amemueleza Rais wa Russia kwamba, nchi hizo mbili zimepata matokeo ya kuridhisha katika vita vya kupambana na ugaidi wa kimataifa.