IQNA

Erdogan: Kadhia ya Quds inawahusu Waislamu bilioni 1.7 duniani

16:51 - September 23, 2019
Habari ID: 3472145
TEHRAN (IQNA) – Rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki, ambaye yuko New York kuhudhuria mkutano wa 74 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa amesema nchi yake itaendelea kuunga mkono harakati za ukombozi wa Palestina.

"Palestina ni mstari mwekundu kwa Uturuki," amesema Erdogan akizungumza wiki hii katika mkutano na wawakilishi wa jamii ya Waislamu Marekani.

Rais wa Uturuki alisisitiza kuhusu haja ya kulinda haki za Wapalestina na kuunga mkono ukombozi wa mji wa Quds Tukufu (Jerusalem) na kuongeza kuwa, "hakuna dola lolote kubwa linaloweza kutuzuia kulinda haki za Palestina."

Ameongeza kadhia ya Quds Tukufu ni kadhia ya Waislamu wachache tu wa Palestina bali inahusu heshima na hadhi ya Waislamu bilioni 1.7 kote duniani.

"Tunaamini kuwa kutetea Quds Tukufu ni kutetea thamani za ubinadamu, amani na uadilifu," amesema Erdogan.

Ikumbukwe kuwa Disemba mwaka 2017, Rais Donald Trump wa Marekani aliutambua mji wa Quds kuwa eti ni mji mkuu wa utawala haramu wa Israel na kutangaza kuuhamishia ubalozi wa Marekani katika mji huo.

Aidha hivi karibuni kumevuja mpango wa 'Muamala wa Karne' wa Rais Trump wa Marekani wenye lengo la kukandamiza kabisa haki za taifa la Palestina kwa maslahi ya utawala haramu wa Israel.

Msikiti wa Al-Aqsa, kibla cha kwanza cha Waislamu, uko katika mji wa Quds na utawala wa Kizayuni wa Israel unatekeleza njama za kuubomoa msikiti huo ili hatimaye kuuyahudisha kikmilifu mji wa Quds.

Wapigania ukombozi wa Palestina wameapa kuendeleza mapambano hadi utakapokombolewa kikamilifu mji huo na ardhi zote za Palestina zinazokaliwa na utawala wa Israel.

3844262

captcha