IQNA

Dar al-Ifta ya Misri

Inajuzu Waislamu kuwapongeza Wakristo katika Siku Kuu ya Krismasi

19:07 - December 16, 2018
1
Habari ID: 3471773
TEHRAN (IQNA)- Huku Wakristo wakikaribia kusherehekea uzawa wa Nabii Isa AS (Yesu) katika siku ya Krisimasi na pia mwaka mpya Miladia, Taasisi ya Dar al-Ifta ya Misri imesema inajuzu au ni sawa kwa Waislamu kuwapongeza wasiokuwa Waislamu kwa munasaba wa siku kuu zao na kwamba hilo ni kwa mujibu wa mafundisho ya dini tukufu ya Kiislamu.

Kwa mujibu wa ripoti ya IQNA, Tovuti ya Al Ahram imeripoti kuwa, Dar al-Ifta ya Misri, inayoshughulikia masuala ya fatuwa za Kiislamu, imetangaza kuwa: "Mafundisho ya dini ya Kiislamu yanawahimiza Waislam kutoa salamu za pongezi kwa wasiokuwa Waislamu katika idi na minasaba yao ya kidini na hili ni kwa mujibu wa ubora wa tabia njema ambazo alikuja nazo Mtume SAW."

Dar al-Ifta ya Misri imeambatanisha taarifa hiyo na ujumbe wa video kuhusu kuwapatia wafuasi wa dini zingine salamu za pongezi kwa munasaba wa kumbukumbu za kuzaliwa manabii wao. Dar al-Ifta ya Misri imesema Uislamu ni dini inayowahimiza watu kuishi pamoja kwa maelewano na kwamba hakuna kosa kuwapa wasiokuwa Waislamu zawadi na kupokea zawadi zao kwa minasaba hiyo.

Dar al-Ifta ya Misri imeongeza kuwa kumbukumbu za uzawa wa Manabii wa Mwenyezi Mungu ni kheri na amani kwa wanaadamu wote na Uislamu ni dini ya amani, rehema, ubora na watu kutembeleana na kujuliana hali. Aidha ujumbe huo umeashiria Aya ya 107 ya Suratul Anbiyaa isemayo: "Nasi hatukukutuma ila uwe ni Rehema kwa walimwengu wote."

Katika ujumbe wake wa video, Dar al-Ifta ya Misri imetoa wito kwa Waislamu kufuatia Sira ya Mtume Muhammad SAW na kuwataka wasitumbukie katika mitego ya makundi ya wenye misimamo mikali ya kufurutu ada ambao wanawakufurisha wale wote wasioafiki fikra zao finyu.

3772252

Imechapishwa: 1
Inatathminiwa: 0
Haiwezi kuchapishwa: 0
Hassan Ali
0
0
Inabidi kuanza kufanya utafiti wa kindani zaidi kabla ya kukubali au kukataa.
captcha