IQNA

Umoja wa Mataifa walaani hatua ya Bahrain kuwanyonga wapinzani

9:41 - July 31, 2019
Habari ID: 3472065
TEHRAN (IQNA)- Umoja wa Mataifa umelaani vikali hatua ya utawala wa Aal Khalifa huko Bahrian kuwanyonga vijana wawili wapinzani.

"Tunalaani vikali kunyongwa raia wawili wa Bahrain, Ali Mohamed Hakeem al Arab, 25 na Ahmed Isa al Malali, 24 mnamo Julai 26 mjini Manama. Wamenyongwa Ijumaa usiku pamoja na kuwa Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu (wa UN) alibainisha wasiwasi wake kufuatia taarifa za wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa. Watu hao 'walikiri' kufanya makosa baada ya kunyongwa na wala mfumo wa sheria haukufuatwa ili kesi yao isikilizwe kwa haki na uadilifu. Mtu mwingine, mfanyakazi wa kigeni, pia alinyongwa baada ya kupatikana na hatua ya mauaji, alisema msemaji wa Tume ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa, Rupert Colville, akizungumza Jumanne mjini Geneva Uswisi. Amesema Umoja wa Mataifa una wasiwasi kuhusu wafungwa waliohukumiwa kunyongwa nchini Bahrain na ameutaka utawala wa nchi hiyo kusitisha unyongaji huo.
Utawala wa kiimla wa Aal-Khalifa umewanyonga vijana hao licha ya mashirika ya kutetea haki za binadamu yakiwemo ya Amnesty International na Human Rights Watch pamoja na Umoja wa Mataifa kutoa miito hapo jana ya kutaka kusimamishwa utekelezaji wa adhabu hiyo ya kifo.
Shirika la Human Rights Watch limesema, mahakama za Bahrain haziko huru na zinatoa hukumu kiuonevu na kubainisha kuwa, mahakama hizo ndio mkandamizaji mkuu wa raia kwa kutoa hukumu za kidhalimu na kiuonevu kwa watu wanaoandamana kwa amani.
Tangu Februari mwaka 2011, wakati ulipoanza mwamko wa Kiisamu Asia Magharibi, Bahrain imekuwa uwanja wa maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa.
Wananchi hao wanataka kuwepo uhuru, utekelezwe uadilifu, ukomeshwe ubaguzi na kuundwa serikali itakayochaguliwa na wananchi wenyewe.
Hata hivyo kwa msaada wa wanajeshi wa Saudi Arabia na askari usalama wa Imarati waliotumwa nchini Bahrain kupitia mpango wa ulinzi wa Ngao ya Kisiwa, utawala wa Aal Khalifa unatumia mkono wa chuma kukabiliana na matakwa ya wananchi hao.
Kwa mujibu wa duru za haki za binadamu, Bahrain ina idadi kubwa zaidi ya wafungwa wa kisiasa kulinganisha na idadi ya watu katika nchi hiyo ndogo zaidi katika Ghuba ya Uajemi.

3469084

Kishikizo: iqna bahrain aal khalifa
captcha